Thursday 29 June 2017

WIZARA YATAKA BIASHARA YA TANZANITE IFANYIKE SIMANJIRO….

Wizara ya Nishati na Madini, imeagiza biashara ya madini ya Tanzanite, ifanyike katika Halmashauri ya Simanjiro na siyo Arusha na Moshi kama inavyofanyika hivi sasa.

Naibu Waziri wa wizara hiyo Dk Medard Kalemani, alitoa agizo hilo mjini Babati kama njia mojawapo ya kuhakikisha ulipaji wa kodi na kudhibiti utoroshwaji wa madini hayo, yanapatikana eneo la Mirerani, wilayani Simanjiro pekee.
Alikuwa akizungumza na wachimbaji wakubwa na wadogo, pamoja na wanunuzi, katika kikao kilichofanyika ukumbi wa Mkoa wa Manyara Jumamosi iliyopita.
Alisema haiingii akilini kuona wananchi wa Wilaya ya Simanjiro wakiishi katika hali ya kukosa mahitaji ya lazima kama maji safi, shule zilizokamilika na badala yake wananchi kuwa katika maisha duni ilhali wilaya hiyo ina utajiri mkubwa, badala yake wanufaika wa madini hayo ni watoroshaji na wananufaisha nchi nyingine.

Mkuu wa Wilaya ya Simanjiro, Zephania Chaula, alisema wilaya hiyo ina wachimbaji wa madini zaidi ya 2,000 ambao hawalipi kodi, na kwamba halmashauri ya wilaya hiyo inapoteza mapato mengi kwa kuwa fedha inayopata inatokana na mchanga wa madini na si madini yenyewe.

0 comments:

Post a Comment