Monday 23 April 2012

Zijue faida za ajabu za kula karanga..!


Wengi wetu huchukulia ulaji wa karanga kama chakula cha kujiburudisha na kisichokuwa na umuhimu sana katika afya ya mwili wa binadamu. Kiukweli karanga siyo chakula cha kupuuziwa iwapo utajua faida zake kama nitakavyokujuza leo katika makala haya.

MAGONJWA YA MOYO....


Kama ilivyokuwa kwa korosho, karanga nazo ni chanzo kizuri cha mafuta mazuri aina ya ‘monounsaturated fats’ ambayo yanatiliwa mkazo kutumiwa kwa afya ya moyo. Kwa mujibu wa utafiti, watu wanaokula karanga mara kwa mara hupunguza hatari ya kupatwa na ugonjwa wa moyo (cardiovascular heart disease) kwa asilimia 21.

Aidha, katika taarifa iliyochapishwa kwenye jarida moja la Uingereza la ‘Journal of Nutrition’ ambako kuna matokeo ya taarifa nne za utafiti, imeonesha pia watu wanaotumia karanga mara kwa mara, angalau mara nne kwa wiki, hujipa kinga nyingine dhidi ya ugonjwa wa moyo (coronary heart disease) kwa zaidi ya asilimia 37.

Mbali ya kuwa na mafuta mazuri yanayotoa kinga kwenye moyo, karanga pia, hasa za kukaanga, zinaelezwa kuwa na kiwango kikubwa cha virutubisho vinavyotoa kinga ya mwili (antioxidants) kuliko hata kile kinachopatikana kwenye tunda la epo na karoti!

Ili kupata kinga hiyo dhidi ya aina hizo mbili za ugonjwa wa moyo, ambao unatesa watu wengi duniani na kugharimu pesa nyingi kwa matibabu, unashauriwa kula karanga pamoja na bidhaa zake kama vile ‘peanut butter’, angalau kijiko kimoja cha chakula, mara nne kwa wiki.

KINGA DHIDI YA KIHARUSI......


Ugonjwa mwingine hatari unaosumbua watu wengi hivi sasa ni kiharusi au ‘stroke’, lakini unaweza kujikinga nao kwa kuwa na mazoea ya kula karanga tu.

Utafiti umeonesha kuwa karanga ina kirutubisho aina ya ‘Resveratrol’ ambacho hupatikana pia kwenye zabibu na mvinyo mwekundu (red wine).

Kwa mujibu wa utafiti uliofanywa maabara na kuchapishwa kwenye jarida la Kilimo na Kemia ya Chakula (Journal of Agricultural Food Chemistry), umeonesha kuwa kirutubisho hicho huimarisha utembeaji wa damu kwenye mishipa inayokwenda kwenye ubongo kwa kiasi cha asilimia 30.

KINGA DHIDI YA KANSA YA TUMBO....


Faida nyingine inayoweza kupatikana kwenye mwili kutokana na ulaji wa karanga, ni kinga dhidi ya ugonjwa wa saratani ya tumbo.

Kwa mujibu wa utafiti uliofanywa, unaonesha kuwa virutubisho vya ‘folic acid’, ‘phytosterols’, ‘phytic acid’ (inositol hexaphosphate) na resveratrol’ vinavyopatikana kwenye karanga, huweza kutoa kinga dhidi ya ugonjwa wa saratani ya tumbo.

Zaidi utafiti huo umeonesha kuwa ulaji wa karanga, hata mara mbili tu kwa wiki, una uwezo wa kupunguza uwezekano wa kupatwa na saratani ya tumbo kwa asilimia 58 kwa wanawake na asilimia 27 kwa wanaume!

Kwa maelezo hayo kuhusu faida za karanga mwilini, bila shaka chakula hiki kinapaswa kupewa kipaumbele katika orodha ya vyakula tunavyokula kila siku na hakika Mungu ametupenda sana kwa kutupa kinga dhidi ya maradhi yote yanayotukabili kwa njia ya vyakula.

By kiwa strong.....

0 comments:

Post a Comment