Shirika la Maendeleo ya Kimataifa la Marekani (USAID) ambao hutumiwa na
Marekani kutoa misaada kwa nchi za nje, limesitisha ufadhili wake kwa miradi ya
afya nchini Kenya.
Taarifa kutoka kwa
shirika hilo imesema hatua ya kusitisha ufadhili kwa miradi yote ya Wizara ya
Afya ya Kenya imetokana na hatua ya Kenya kutotimiza "masharti ambayo
hayajaelezwa".
Maafisa wa USAID
wameagizwa kutojishughulisha na "shughuli zozote za kibiashara" na
taasisi za serikali ya Kenya pamoja na mashirika mengine yenye uhusiano na
serikali.
Hatua hiyo ya Marekani
inatarajiwa kuathiri miradi mbalimbali ya serikali ikiwemo mipango ya
kukabiliana na malaria, kifua kikuu na Ukimwi pamoja na miradi ya uzazi wa
mpango, huduma za afya kwa wajawazito na watoto.
Kwa miezi kadha sasa,
wizara ya afya nchini Kenya imekubwa na tuhuma za ulaji rushwa.
Sekta ya afya Kenya
pia ilitatizwa na mgomo wa taifa madaktari ambao ulidumu kwa siku 100 kuanzia
Desemba.
Mwaka uliopita,
mkaguzi mkuu wa hesabu za serikali alisema jumla ya dola 50 milioni
hazikubainika zilivyotumiwa katika wizara ya afya.
Maafisa wakuu katika
wizara ya afya pamoja na jamaa za baadhi ya viongozi wakuu serikalini walidaiwa
kuhusika katika kufujwa kwa pesa hizo.
Wizara ya afya hata
hivyo ilijitetea na kusema madai hayo yalikuwa kwenye ripoti ambayo
ilifichuliwa mapema kabla ya wahasibu wa wizara hiyo kujibu maswali yaliyokuwa
yameibuliwa na mkaguzi huyo kuhusu matumizi ya pesa hizo.
Mwandishi wa BBC
Abdinoor Aden anasema hatua ya sasa hivi ya serikali ya Marekani itaibua
maswali zaidi kuhusu usimamizi wa fedha katika Wizara ya Afya Kenya licha ya
hatua ya rais Kenyatta ya kumhamisha Katibu Mkuu wa wizara hiyo.
Hatua ya USAID
inatarajiwa kuathiri sana miradi ya serikali pamoja na miradi ya mashirika
mengine ya afya ambayo hutumiwa an USAID kutoa huduma maeneo mbalimbali Kenya.
0 comments:
Post a Comment