Kufuatia tishio la kuwapo
programu mtumishi (software) yenye virusi aina ya WannaCry, Mamlaka ya
Mawasiliano Tanzania (TCRA) imetoa onyo kwa watumiaji wa kompyuta kutofungua
viambatanishi wasivyovijua kwenye barua pepe zao.
Aidha, taasisi zimetakiwa kutunza
data nje ya mtandao ili kuepuka athari endapo kompyuta zitashambuliwa na virusi
hivyo, sambamba na kuhuisha mifumo ya ulinzi dhidi ya virusi.
Mkurugenzi Mkuu wa TCRA, James Kilaba alibainisha kuenea kwa
programu mtumishi hiyo yenye virusi vinavyoathiri na kumzuia mtumiaji kufikia
mafaili au mifumo, ama kwa kufungia mifumo ya screen au kuharibu faili kwenye
kompyuta.
“Likitokea tatizo hilo hackers (wadukuzi) wanadai kiasi fulani
cha fedha ili kuweza kuzipata faili kwenye kompyuta. Kulipa hizo fedha hakukupi
hakikisho la kupata mafaili yaliyoathirika, hivyo tunawashauri watumiaji na
taasisi kutolipa fedha.” “Endapo mtumiaji au taasisi wanakumbwa na tatizo hilo
basi watoe taarifa kwa Timu ya kitaifa ya dharura ya kompyuta (TZCERT),”
alisema.
Kilaba alisema tishio la virusi WannaCry haliko kwenye kompyuta
pekee bali pia kwenye simu za kisasa endapo utafungua kiambatanisho au link
yenye virusi hivyo.
Kilaba alisema virusi WannaCry kinaharibu programu za kwenye
kompyuta zilizopitwa na wakati au software zenye shida hususani Microsoft
Server Message Block 1.0 (SMBv1) zilizotolewa mapema mwaka huu na Microsoft
kama njia ya kuzuia mazingira magumu na watumiaji wa Microsoft wanaweza kuokoa
kompyuta zao kwa kuweka njia za usalama.
0 comments:
Post a Comment