Pamoja na
maendeleo yaliyotokana na kukua kwa pato la wastani la Mtanzania na kupungua
kwa
umasikini wa mahitaji ya msingi, serikali imeainisha mikoa mitano
iliyokithiri kwa umasikini wa kipato.
Akiwasilisha bungeni Taarifa ya Hali ya Uchumi ya 2015 na
Mpango wa Maendeleo wa Taifa 2016/17, Waziri wa Fedha na Mipango Dk Philip
Mpango, amesema mkoa unaoongoza ni Kigoma ambao wakazi wake asilimia 48.9,
wanakabiliwa na umasikini uliokithiri wa kipato.
Mikoa mingine yenye umasikini wa kipato ni Geita (asilimia
43), Kagera (asilimia 39), Singida (asilimia 38.2) na Mwanza (asilimia 35.3).
Katika
wilaya zilizokithiri kwa umasikini wa kipato, ni Kakonko mkoani Kigoma na
Biharamulo mkoani Kagera, ambapo Dk Mpango amesema katika wilaya hizo,
takribani asilimia 60 ya watu wake, wako chini ya mstari wa umasikini wa
mahitaji ya msingi.
Tathmini ya hali ya umasikini kimaendeleo iliyoainisha
umasikini huo, imetumia takwimu za Sensa ya Watu ya mwaka 2012 na Utafiti wa
Hali ya Kipato na Matumizi katika Kaya wa 2012, ulionesha pia ahueni ya
umasikini katika mikoa mitano.
Dk Mpango ametaja mikoa hiyo yenye ahueni na idadi ya watu
wanaokabiliwa na umasikini wa kipato katika mabano kuwa ni Dar es Salaam
(asilimia 5.2), Kilimanjaro (asilimia 14.3), Arusha (asilimia 14.7), Pwani
(asilimia 14.7) na Manyara (asilimia 18.3).
Pamoja na
tathmini ya kimkoa na kiwilaya lakini katika nchi nzima, amesema kati ya mwaka
2010 na 2015, Pato la Mtanzania liliongezeka kutoka Sh 770,464.3 kwa mwaka
mpaka Sh milioni 1.9 mwaka 2015 sawa na mara 2.5.
0 comments:
Post a Comment