Tuesday 7 June 2016

MBEGU ZA KIUME ZENYE UKIMWI KUSAFISHWA NCHINI..!

Wanaume wanaoishi na virusi vya Ukimwi sasa huenda wakapata suluhisho, la kupata
watoto na wenza wao ambao hawana virusi hivyo, baada ya kuwapo tiba ya kusafisha mbegu za kiume zenye VVU hapa nchini.
Tiba hiyo sasa inapatikana hapa nchini katika hospitali moja iliyo jijini Dar es Salaam, ambayo inatoa huduma za uzazi na upandikizaji wa mimba katika mirija ya uzazi kitaalamu inayojulikana In Vitro Fertilization (IVF).
Kwa sasa, njia ya kuzuia maambukizi ya VVU kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto (MTCPT) ndiyo inayotumika duniani kote, kwa mjamzito kupewa dawa za ARV wakati wa ujauzito zinazokinga maambukizi kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto na baada ya mtoto kuzaliwa.
Kadhalika mtoto hutakiwa kunyonya maziwa ya mama pekee kwa kipindi cha miezi sita au kutonyonya kabisa ili asipate maambukizi.
Tovuti ya hospitali inayotoa huduma hizo, inaeleza kuwa wanatoa huduma hiyo ya kusafisha mbegu za kiume zenye VVU na kisha kuzipandikiza kwa mwanamke asiye na VVU kwa njia ya IVF.
Shirika la Afya la Kimataifa (WHO), liliwahi kuchapisha utafiti wa kuosha mbegu za kiume na kueleza kuwa matibabu hayo yanawezekana, ingawa si kwa asilimia 100.
Katika utafiti wa WHO, wenza 914 walipimwa baada ya mbegu za kiume kuoshwa. Kati ya hao, wanawake walipopimwa baada ya kupata ujauzito hawakuonekana na VVU, wala watoto hawakuonekana kuwa na maambukizi hayo.
Kadhalika WHO walieleza kuwa matokeo ya utafiti huo yalionyesha kuwa kati ya asilimia 1 hadi 20 ya mbegu zilizooshwa na kupandikizwa kwa wanawake, bado zilikuwa na VVU. (yaani kesi 70 kati ya sampuli 1279)
Wanasema mbinu hiyo ya kusafisha inahusisha mchakato mrefu, ikiwamo kupima zaidi ya mara kumi sampuli za mbegu zilizosafishwa.
Hata hivyo WHO wamesema kuosha mbegu za kiume kunapunguza hatari ya maambukizi, lakini hakuwezi kuondoa kabisa VVU ndani ya mbegu hizo.
Hospitali
Tovuti ya kliniki hiyo inaeleza wazi huduma zinazotolewa ambapo mbali na uchangiaji wa mbegu na mayai, lakini huduma kuu ni kuwasaidia wenye matatizo ya uzazi, kupata watoto kwa njia ya upandikizaji.
Huduma nyingine ni kutibu matatizo ya ugumba kwa wanawake na wanaume, kuchagua jinsia ya mtoto, upasuaji wa kukaza kizazi kuzuia mimba kutoka (shridkar shuture) pamoja na huduma za uzazi.
Kuchangia mbegu au mayai ni katika kuhakikisha hakuna upungufu wa mbegu, na kuwasaidia wale wote ambao wameshindwa kutimiza ndoto za kuwa na familia.
Jinsi mbegu zinavyooshwa
Kisayansi, damu pekee si kipimo cha kuonyesha kuwapo kwa maambukizo ya VVU katika mwili bali hata katika majimaji ya mwilini.
Ogani zinazozalisha majimaji ya mbegu za kiume, huathiriwa kwa namna ya pekee na VVU.
Daktari Bingwa wa Uchunguzi wa magonjwa, Henry Mwakyoma alisema kwa kawaida virusi vya Ukimwi hupenda kukaa katika chembehai nyeupe(CD4).
Alisema ndiyo maana inawezekana mwanamume mwenye VVU, asimwambukize mwenza wake.
Hata hivyo, Dk Mwakyoma aliona kuna ugumu kuzisafisha mbegu za kiume na kuondoa majimaji yake yenye VVU, ili kuzipandikiza mbegu hizo ili zitungishe mimba kama unavyosema utafiti huo.
Daktari wa Kitengo cha Uchunguzi wa magonjwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, Innocent Mosha anaungana na Dk Mwakyoma na kusema, kwa kawaida mbegu za kiume hazina VVU kwa sababu ni seli inayojitegemea, lakini majimaji yanayobeba mbegu hizo ndiyo huwa na VVU.
Wanasayansi wanasema mwanamume anaweza asionyeshe VVU katika damu, lakini majimaji ya mbegu za kiume yakaonyesha uwapo wa virusi.
Wanaeleza kuwa kwa mwanamume anayetumia dawa za kufubaza makali ya VVU, majimaji hayo yakipimwa hayaonyeshi uwapo wa VVU, bali virusi huonekana katika damu tu. Hii ni kwa sababu ARV hupunguza wingi wa virusi na hivyo kushuka na kufikia kiwango cha kutoonekana.
Jarida la Science Daily la nchini Uingereza linaonyesha robo tatu ya wanaume wanaoishi na VVU na wanaotumia ARV, walipopimwa majimaji yanayobeba mbegu za kiume hayakuwa na VVU.
Hata hivyo, utafiti uliofanywa mwaka 2009 na Jarida la Tiba la nchini Canada ulibaini kuwa mbegu za kiume zina nafasi kubwa ya kusambaza virusi vya Ukimwi.
Utafiti huo ulikinzana na huu wa usafishwaji wa mbegu hizi, kuondoa majimaji ambayo kwa kawaida ndiyo hudhaniwa kubeba VVU.
Matokeo ya utafiti huo yalionyesha kuwa mbegu za kiume zina nafasi kubwa ya kusambaza VVU wakati wa tendo la ndoa, kwani virusi hivyo hujichimbia katika chembehai nyeupe ambazo utafiti ulisema ipo katika mbegu za kiume.


Utafiti huo ulikanusha tafiti za awali ambazo zinathibitisha kuwa ni majimaji tu yanayobeba mbegu hizo ndiyo yenye kuathiriwa na VVU.
Source Mwananchi news Paper

0 comments:

Post a Comment