Wakazi wa Kijiji cha
Nditu, Kata ya Suma, Wilaya ya Rungwe mkoani Mbeya,
wamegoma
kuzika mwili wa marehemu Shabani Yusufu (27), baada
kushambuliwa na kundi la siafu nyumbani kwake na kusababisha
apoteze uhai.
Yusufu amefariki dunia ikiwa
ni siku moja tu baada ya kufunga ndoa na kuzua gumzo kubwa kijijini hapo, jambo
ambalo linahusishwa na imani za kishirikina.
Akisimulia mkasa huo baba mzazi wa
marehemu Ebron Mwaipaja, amesema mwanawe alitoka kufunga ndoa juzi na
alikutwa na mauti hayo akiwa amejipumzisha chini ya mti nyumbani kwake, ambako
ghafla alivamiwa na siafu.
Amesema kulikuwa na maneno ya
hapa na pale wakati wa maandalizi ya harusi hiyo kutoka kwa baadhi ya watu, ambayo
yamesababisha tukio hilo kuhusishwa na imani za kishirikina.
Baba huyo amesema baada ya
tukio hilo, wananchi na uongozi wa Serikali ya kijiji walifika eneo hilo, huku
wakimtaja mmoja wa wanakijiji kuwa ndiye aliyetuma siafu hao.
Amesema wananchi waligoma
kuandaa taratibu za mazishi wakishinikiza aletwe mganga wa jadi apige ramli,
ili kumbaini mtu anayeendesha matukio ya ushirikina yanayoendelea kijijini hapo.
Ameeleza kuwa baada ya
wananchi kugoma kuzika serikali ya kijiji nayo iligoma kutoa kibali ili mganga
aitwe, ikisema siku zote Serikali haiamini uchawi, jambo ambalo lilisababisha
wananchi waliokuwa na silaha za jadi, kufanya maandamano na kufunga barabara.
0 comments:
Post a Comment