Thursday 31 December 2015

Gereza kuvunjwa ili madini yachimbwe….!


Gereza la Songwe mkoani Mbeya linatarajiwa kuvunjwa na kujengwa sehemu nyingine kupisha uchimbaji wa madini adimu duniani ya niobium.

Ni baada ya madini hayo kugundulika kuwapo kwenye eneo la gereza hilo,endapo utaanzishwa mgodi wa madini hayo utakuwa wa pili katika Bara la Afrika baada ya Nigeria.
Taarifa za uhakika zimeonyesha michoro ya ujenzi wa gereza jipya imeandaliwa.
Mhandisi wa Migodi wa Kanda ya Kusini Magharibi, Zephania Nsungi alisema Kampuni ya Panda Hill Niobium Project Tanzania imefanikiwa kupata madini hayo karibu na gereza hilo.
Madini hayo ni adimu duniani na yanapatikana katika nchi chache sana, hivyo yakianza kuchimbwa upo uwezekano wa kuliondoa Gereza la Songwe na kujengwa upya eneo jingine.
Mfanyakazi wa kampuni hiyo Emmanuel Kisasi alisema kwamba, viongozi wao wako likizoni Ulaya na wanatarajia kurejea nchini mwezi ujao.
Kisasi ambaye hakutaka kuzungumza kwa kina juu ya madini hayo, alithibitisha kuwapo kwa mpango wa kuanza kwa mgodi eneo hilo na kwamba, unatarajiwa kudumu kwa zaidi ya miaka 30.
Mkuu wa Magereza mkoani humo Julius Sang’udi naye alithibitisha kuwapo kwa mpango huo na kusisitiza kwamba, unasimamiwa na Wizara ya Nishati na Madini kwa kushirikiana na Jeshi la Magereza chini ya Kamishna aliyemtaja kwa jina moja la Chamlesile.
Kwa mujibu wa taarifa za mtandao, madini hayo huchanganywa na metali zingine na vyuma vyake hutumika kwenye ujenzi wa bomba la kupitishia mafuta.
Vilevile hutumika kama metali kwa injini za ndege na husaidia kuzuia mitambo yake kutopata joto kali.

0 comments:

Post a Comment