Bunge la Zambia limemsimamisha kazi Waziri wa Jimbo la Lusaka Bowman
Lusambo kwa muda wa mwezi mmoja, baada ya kumchapa kibao mbunge Chishimba Kambwili
wakiwa bungeni.
Spika wa Bunge hilo amesema ni jambo la kawaida wabunge kutumia lugha
isiyofaa na kuleta mizozo, lakini kwa kitendo cha Waziri kumpiga kibao mbunge
ni kitendo kisicho vumilika.
Patrick Matibini ambaye ni spika wa Bunge hilo, amesema kitendo hicho
kilifanyika Oktoba mwaka jana na kuongezea kwamba tabia hiyo haikubaliki kamwe.
Kufuatia adhabu hiyo Waziri Lusambo atasitishiwa baadhi ya huduma
zinazotolewa bungeni kama marupurupu na mshahara, kwa muda wa kipindi chote
atachokuwa anatumikia adhabu hiyo.
Aidha
imeelezwa kuwa mbunge huyo aliyepigwa kibao amekuwa akiwatukana maofisa wa
Serikali kwa tuhuma za rushwa tangu atolewe kuwa Waziri wa Mawasiliano mwaka
2016, japo Serikali imekuwa ikikanusha tuhuma hizo.
Hata
hivyo imeelezwa kuwa Waziri huyo alichukua sheria hiyo mkononi ya kumchapa
kibao mara mbili baada ya kuona mbunge huyo anazungumza uongo juu ya Serikali.
0 comments:
Post a Comment