Thursday 24 September 2015

Upinzani wavalia sare za wanafunzi Kenya………

Wabunge na maseneta walivalia mavazi yanayofanana na sare za wanafunzi
Baadhi ya viongozi wa upinzani nchini Kenya wamevalia mavazi yanayofanana na sare za wanafunzi wakiitaka serikali kulipa walimu nyongeza ya mishahara.

Walimu wamekuwa mgomoni tangu kufunguliwa kwa muhula wa tatu na Serikali ilifunga shule zote za umma Jumatatu.
Mrengo wa Coalition for Reforms and Democracy (Cord) unaoongozwa na Raila Odinga jana iliandaa mkutano wa kisiasa uwanja wa Uhuru Park, Nairobi kuishinikiza serikali iwalipe walimu nyongeza ya asilimia 50 hadi 60 kama ilivyoagizwa na mahakama.
"Kuna pesa za kutosha, lakini zinapotea kwa ufisadi. Uhuru (Rais Kenyatta) anafaa kushauriana na walimu. Asiseme hawezi kulipa na hatalipa," alisema Bw Odinga.
Kiongozi wa chama cha Wiper Kalonzo Musyoka alisema "pesa zipo" za kuwalipa walimu.

Mgomo huo wa walimu unatishia kutatiza mitihani ya kitaifa ambayo inatarajiwa kuanza wiki chache zijazo.
Kwa mujibu wa Baraza la Kitaifa la Mitihani Kenya (KNEC) kuna watahiniwa 937,467 wanaojiandaa kufanya mtihani wa darasa la nane KCPE utakaoanza Novemba 10 na kumalizika Novemba 12.
Watahiniwa wanaojiandaa kufanya mtihani wa kidato cha nne KCSE utakaoanza rasmi Oktoba 12 ni 525,802.
Baraza hilo limesema mitihani hiyo haitaahirishwa.

0 comments:

Post a Comment