Thursday 9 March 2017

HILI NDIO CHIMBUKO LA SIKU YA WANAWAKE DUNIANI.....

Leo tarehe 8 Machi, 2017 dunia zima inaadhimisha Siku ya Wanawake Duniani, ambayo huadhimishwa kila mwaka kwa lengo la kutambua na kuthamini mchango wa mwanamke katika jamii. Chimbuko la kuanzishwa kwa Siku ya Wanawake lilianza mwanzoni mwa
miaka ya 1900 kufuatia maandamano ya wanawake wafanyakazi wa sekta ya viwanda nchini Marekani kupinga mazingira duni ya kazi.
Waandamaji hao, walilalamikia ukosefu wa huduma za kijamii na kuwepo kwa vitendo vya unyanyasaji katika ajira ikiwemo wanawake kulipwa mshahara mdogo kwa kazi sawa ukilinganisha na wanaume.
Kwa kuzingatia hali hiyo, Umoja wa Mataifa baada kuanzishwa mwaka 1945 uliridhia kuwa tarehe 8 Machi kila mwaka iwe ni Siku ya Kimataifa ya Wanawake Duniani.

Uamuzi wa Umoja wa Mataifa wa kuanzisha Siku ya Wanawake Duniani ulitokana na ukweli kwamba masuala ya haki, maendeleo na usawa wa wanawake yalihitaji msukumo maalumu na wa kipekee.

Lengo kuu la kuadhimisha Siku ya Wanawake Duniani ni kutoa fursa kwa jamii kupima utekelezaji wa maazimio, matamko, mikataba na itifaki mbalimbali za Kimataifa, kikanda  na kitaifa zinazohusu masuala ya maendeleo ya jinsia na uwezeshaji wanawake.
Hii ni pamoja na kuhakikisha kuwa haki za wanawake kiuchumi, kijamii, kiutamaduni na kisiasa zinapatikana na zinalindwa.
Kuadhimisha Siku ya Wanawake Duniani ni kuhamasisha jamii kuhusu umuhimu wa kutambua na kuthamini uwezo na mchango mkubwa wa wanawake katika kuleta maendeleo pamoja na kuelezea jitihada mbalimbali zilizofanywa na Serikali na wadau mbalimbali katika kuwajengea uwezo wa kiuchumi na kijamii ili waweze kushiriki kikamilifu katika kujiletea maendeleo yao, familia zao, jamii na Taifa kwa ujumla.

Kwa Tanzania wanawake ni kundi kubwa na muhimu katika jamii (asilimia 51 ya Watanzania Wote) hivyo hakuna maendeleo yeyote yanayoweza kufikiwa ikiwa kundi hili litaachwa nyuma.

0 comments:

Post a Comment