Saturday 11 March 2017

TANZANIA NI NCHI YA MWISHO ULAJI NYAMA A. MASHARIKI…

Pamoja na kwamba Tanzania ni moja ya nchi zenye mifugo mingi barani Afrika, watanzania wanakula nyama kwa kiwango kidogo ikilinganishwa na nchi nyingine za Afrika ya Mashariki.

Mtanzania anakula kilo 15 kwa mwaka, wakati nchi jirani ya Kenya, mtu anakula kilo 17, Sudan 21 na Bostwana kilo 27.3 kwa mwaka.
Kiwango hicho cha ulaji wa nyama cha Tanzania na nchi hizo nyingine bado ni mdogo ukilinganisha ni kilichowekwa na Shirika la Chakula la Umoja wa Mataifa (FAO) cha ulaji wa wastani wa kilo 50 kwa mwaka kwa mtu.
Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi (Uvuvi), Maria Mashingo alitoa msisitizo huo mjini hapa wakati akifungua mkutano wa wajumbe wa Baraza la Wadau wa Tasnia ya Nyama nchini.
Maria aliwataka wadau hao kuzisajili kazi zao ili zitambuliwe na watumie mizani ya kisasa (ya kidigitali) na mashine za kukata nyama ili kuwezesha wajali kununua nyama kwenye vipimo vinacholingana.
“Nasisitiza matumizi ya mizani ya kisasa na mashine za kukatia nyama … ili kuwezesha wajali kununua nyama kwa kipimo kinacholinga na uwezo wao kifedha,” alisema.
Aliwataka wafugaji hao wafuge kibiashara kwa kunenepesha mifuko na kuvuna kwa wakati ili kupata mifugo bora kwa ajili ya kuzalisha nyama bora. Maria alizitaka sekta binafsi kuwekeza katika ujenzi wa machinjio za kisasa, viwanda vya kusindika nyama na maduka ya nyama yanayokidhi viwango vya ubora.
Alisisitiza kwamba waweke mikakati ya kupunguza kama sio kumaliza kabisa migogoro ya ardhi baina ya wafugaji na watumiaji wa ardhi wengine, kwa kutambua, kutenga na kuendeleza maeneo malisho na maji ya kutosha. Aliwataka pia watumie mizani na kutumia utaratibu wa kuuza mifugo kwa kunadi ili kuwezesha mifugo kupata bei stahili ya mifugo hiyo.
Tanzania ina wastani wa ng’ombe milioni 25.8, mbuzi milioni 17.1, kondoo milioni 9.2, nguruwe milioni 2.67, kuku wa asili milioni 42.0 na wa kisasa milioni 34.5.
Mwenyekiti wa Baraza la Wadau wa Tasnia ya Nyama Tanzania, Doreen Maro alisema, mkutano huo unaongozwa na kaulimbiu ya maendeleo endelevu ya viwanda: Fursa za uwekezaji katika mnyororo wa thamani ya nyama.

Doreen aliahidi kwamba atahamasisha ufugaji wa kibiashara na kuvuna kwa wakati ili kupata mifugo bora inayohitajika katika machinjio na viwanda vya kuzalisha nyama bora na kuongeza thamani ya bidhaa hiyo.

0 comments:

Post a Comment