Wednesday 25 January 2017

FARU MPYA AWEKA REKODI NGORONGORO..!!

Mnyamapori aina ya faru anayesadikiwa kuwa na umri mkubwa kuliko faru wote duniani, anaishi katika hifadhi ya Ngorongoro mkoani Arusha.

Faru Fausta mwenye umri wa miaka 54, ni miongoni mwa faru weusi ambao asili yao ni kusini mwa Afrika na kutokana na umri mkubwa, kwa sasa amepoteza uwezo wa kuona.
Tofauti na faru wengine wenye umri mkubwa duniani, kwa mujibu wa vyanzo mbalimbali, Fausta anaishi katika mazingira ya asili, lakini wengine katika nchi tofauti duniani, ikiwamo Kenya wanaishi katika mazizi maalumu (zoo) au maeneo yaliyotengwa kwa faru yajulikanayo kama “Rhino Sanctuary”.
Mhifadhi Mkuu wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA) Dk. Fred Manongi, amesema kwa sasa Fausta amehifadhiwa katika banda maalumu, baada ya kujeruhiwa na kundi la fisi.
Amesema wataalamu wa wanyamapori na uhifadhi walikuwa wanatafakari kumwachia kutoka katika banda hilo, ili arejee na kuishi kwenye mazingira yake ya asili baada ya afya yake kuimarika.
Kwa upande nchi jirani ya Kenya Desemba 5 mwaka jana, faru mzee kuliko wote nchini humo aliyejulikana kwa jina la Solio (42), alifariki dunia.
Faru ni miongoni mwa wanyamapori ambao wapo katika tishio la kutoweka duniani, kutokana na majangili kuwaua kisha kuuza pembe zao, soko kubwa likiwa Mashariki ya Mbali.

Kwa mujibu wa Taasisi ya Save the Rhino ya nchini Uingereza, kulikuwa na faru laki 5 barani Afrika na Asia mwanzoni mwa karne ya 20, lakini kwa sasa wanakadiriwa kusalia 29,000.

0 comments:

Post a Comment