Wednesday 5 August 2015

Lowassa na Juma Duni, wagombea urais wa UKAWA……

 
Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema),kimemtangaza aliyekuwa Waziri Mkuu wa nchini hiyo Edward Lowassa kuwa mgombea wake wa urais katika uchaguzi mkuu unaotazamiwa kufanyika tarehe 25 Oktoba mwaka huu.


Mkutano Mkuu wa Chadema uliofanyika jana katika ukumbi wa Mlimani City jijini Dar es Salaam, umempitisha Lowassa ambaye wiki iliyopita alikihama chama tawala CCM na kujiunga na chama hicho, kuwa mbeba bendera ya kugombea urais wa Muungano wa vyama vikuu vya upinzani unaojulikana kama UKAWA.

Muungano huo unajumuisha vyama vya Chadema, CUF, NCCR-Mageuzi na NLD.

Katika tukio lisilo la kawaida, Makamu Mwenyekiti wa chama cha CUF Juma Duni Haji ameteuliwa kuwa mgombea mwenza wa urais kwa tiketi ya Chadema.

Duni amelazimika kuchukua kadi ya uwanachama wa chama hicho kwa sababu sheria za vyama vya siasa nchini Tanzania haziutambui muungano wa vyama vya upinzani wa Ukawa kama chama cha siasa.

Wachambuzi wa siasa za Tanzania wamelielezea tukio la leo kuwa ni changamoto kubwa kwa uchaguzi mkuu wa rais wa mwaka huu unaotazamiwa kuwa wa aina yake na ambao utakuwa wa tano kufanyika tangu mfumo wa vyama vingi vya siasa uanzishwe nchini humo mwaka 1992.


 Wakati huohuo mgombea urais kwa tiketi ya CCM John Magufuli, leo alifika ofisi za Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kuchukua fomu za kugombea wadhifa huo huku akisindikizwa na umati mkubwa wa wananchi na wafuasi wa chama hicho.

0 comments:

Post a Comment