Watu watatu wa
familia moja wakazi wa Kijiji cha Mchukwi wilayani Rufiji Mkoa wa
Pwani,
wamekufa baada ya kupigwa na radi jikoni wakati mvua zikinyesha jana jioni.
Inadaiwa kuwa radi hiyo ilianza kupiga mti uliokuwa pembezoni mwa jiko
hilo kabla ya kuwaua ndugu hao.
Shuhuda wa tukio hilo Amina Tenge ambaye pia ni Ofisa Mtendaji wa
kijiji hicho, amesema waliwachukua ndugu hao na kuwapeleka Hospitali ya Misheni
ya Mchukwi kwa ajili ya kupatiwa matibabu ya majeraha waliyopata.
Mganga wa zamu wa Hospital hiyo Esther Mtini, amewataja marehemu hao
kuwa ni Desteria Simba (40), Deborah Simba (2) na Amani Matimbwa (6).
Akizungumzia ajali hiyo Mkuu wa Wilaya ya Rufiji Nurdin Babu, amewataka
wananchi kuepuka kukaa chini ya miti au karibu na miti katika kipindi hiki,
ambacho mvua zinaendelea kunyesha kwani ni hatari kwa maisha yao.
Mamlaka ya Hali ya Hewa (TMA), juzi ilitoa tahadhari ya kuwapo kwa mvua
kubwa zinazoambatana na radi katika baadhi ya mikoa nchini ukiwamo Pwani.
0 comments:
Post a Comment