Sunday 9 April 2017

MBOWE NA MDEE WASEMA WALICHOHOJIWA KWA SAA MBILI.

Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe na Mbunge wa Kawe, Halima Mdee (Chadema), jana wamehojiwa na Kamati ya Kinga, Haki na Madaraka ya Bunge kwa muda wa saa mbili – saa moja kila mmoja.

Wamehojiwa na kamati hiyo baada ya saa 48 tangu Spika wa Bunge, Job Ndugai, atoe agizo la kumtaka Mdee afike bungeni ndani ya saa 24 vinginevyo akamatwe na polisi.
Kuhojiwa kwa wanasiasa hao, kulithibitishwa na Mkurugenzi wa Habari na Mawasiliano wa Bunge, Owen Mwandumbya.
Hata hivyo, Owen alisema hawezi kuzungumza yaliyojiri ndani ya kikao hicho kwa kuwa hakuingia.
Kwa upande wake, Mbowe alisema kamati hiyo ilimuhoji juu ya kauli nne alizotoa usiku wa Jumanne ya wiki hii mbele ya waandishi wa habari, baada ya kumalizika kwa uchaguzi wa wabunge wa Bunge la Afrika Mashariki (EALA), ambao wagombea wawili wa Chadema, Lawrence Masha na Ezekia Wenje, walipigiwa kura za hapana.
Mbowe alisema kauli hizo ni pamoja na aliyosema Ndugai amevunja kanuni na sheria hazikufuatwa katika uchaguzi huo, mchakato wa uchaguzi huo ulikuwa ni mkakati wa Serikali na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, alikuwa anajua, wagombea Chadema walikuwa wazuri lakini kupigwa kura ya hapana ilikuwa ni mkakati wa CCM na ya nne uchaguzi ulikuwa batili.

Naye Mdee alisema alihojiwa juu ya tuhuma zilizotolewa na Ndugai kwamba alitoa kauli za matusi bungeni na suala la pili ni kuzungumza bungeni bila kupewa ruhusa ya Spika.

0 comments:

Post a Comment