Saturday 1 April 2017

PETER LIJUALIKALI ASIMULIA MATESO YA MAGEREZA…

Mbunge wa Jimbo la Kilombero (Chadema) Peter Lijualikali, amesema licha ya mateso makali aliyoyapata akiwa gerezani, amefurahia kifungo hicho kwani kimempa heshima kubwa huku akisema ni kama amepata shahada ya udaktari (Phd).

 

Lijualikali aliyasema hayo jana muda mfupi baada ya kutoka nje ya lango la Gereza la Ukonga jijini Dar es Salaam alikokuwa akitumikia kifungo hicho.
Alielezea hali ya ubaya wa chakula cha gerezani alitolea mfano wa chakula cha dagaa ambao iwapo wakioshwa kiwango cha mchanga ni nusu kikombe. “Tulikuwa tunakula ugali wa dona ambao kwa mtu wa kawaida huwezi kula kwa sababu umechanganywa na magunzi,” alisema.
Alisema ndani ya gereza hilo kuna eneo linaitwa Sitaki Shari ambalo hutumika kutesea wafungwa. Akishuhudia alisema alimwona mfungwa mwenzake ambaye alipigwa katika eneo hilo kiasi cha kutambaa.
Akizungumzia uhusiano wake na maofisa wa magereza, alisema kitaasisi ulikuwa ni mbaya japo kwa askari mmoja mmoja alikuwa akizungumza nao pasipo shida.
Akifafanua alisema kwa hadhi yake yeye kama mbunge alipaswa kulazwa daraja la tatu ingawa aliwekwa katika eneo tofauti na kuliacha daraja hilo wakilazwa watoto wa viongozi, watuhumiwa wa meno ya tembo na raia wa China ambao hakusema walikuwa wanatuhumiwa kwa kesi gani.
“Magereza kuna madaraja matatu, la kwanza, pili na la tatu ambalo nilitakiwa kulazwa humo ili nipewe ulinzi kutokana na hadhi yangu.” Alisema vitendo hivyo na vingine ambavyo hakuvisema atavipeleka ndani ya Bunge Dodoma.
Awali, Lijualikali alieleza kile alichokitaja kuwa ni sababu za kifungo hicho akisema ni msimamo wake wa kukataa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kuchakachua kura kwenye uchaguzi wa Halmashauri ya jimbo hilo.
Alisema msingi hasa wa kifungo hicho ni uhuni na udhalimu uliofanywa na chama hicho dhidi yake kwa kuwa kisheria alitakiwa kuruhusiwa kupiga kura kwa maana yeye ni mbunge halali aliyechaguliwa na wananchi.

Mbali na hilo, Lijualikali aliwalaumu wale aliowaita kuwa ni wenye hekima kukaa kimya kwa kitendo kilichomkuta.

0 comments:

Post a Comment