Mahakama
nchini Korea Kusini imemhukumu bilionea anayetarajiwa kurithi kampuni Samsung
Lee Jae-yong kifungo cha miaka mitano jela kwa makosa ya utoaji rushwa.
Bw Lee alikuwa ameshtakiwa kuhusika
katika rushwa katika kashfa ambayo pia ilichangia kuondolewa madarakani kwa
rais wa zamani wa Korea Kusini.
Kesi hiyo ilikuwa imevutia sana umma
huku hasira zikiendelea kupanda dhidi ya kampuni kubwa za kibiashara za Korea
Kaskazini, maarufu kama chaebols.
Bw Lee, ambaye amekanusha mashtaka
yote, alikuwa amekabiliwa na uwezekano wa kufungwa jela hadi miaka 12.
Bw Lee, ambaye pia hufahamika kama
Jay Y Lee na amekuwa ndiye kiongozi wa kampuni hiyo kubwa zaidi ya kuunda simu
duniani, amekuwa kizuizini tangu Februari akikabiliwa na tuhuma kadha za
rushwa.
Miongoni mwa makosa aliyokabiliwa
nayo ni utoaji rushwa, wizi wa mali ya umma na kuficha mali nje ya nchi.
Lee, 49, pia alituhumiwa kutoa
mchango wa hisani wa won 41bn ($36m; £29m) kwa nyakfu za hisani zilizosimamiwa
na rafiki wa karibu wa rais aliyeondolewa madarakani Park Geun-hye, ndipo
apendelewe kisiasa.
Waendesha mashtaka wanasema mchango
huo ulitolewa kwa mwandani mkuu wa Bi Park ili serikali iunge mkono mageuzi
katika mfumo wa usimamizi wa kampuni ya Samsung ambao ungempatia Lee nguvu
zaidi katika udhibiti wa kampuni ya Samsung Electronics.
Wakili wa Lee amesema tayari kwamba
watakata rufaa uamuzi huo.
Uamuzi huo wa mahakama ni pigo kubwa
kwa kampuni hiyo kubwa zaidi na inayofahamika zaidi ya Korea Kusini.
0 comments:
Post a Comment