Friday 25 August 2017

MKUU WA SAMSUNG AFUNGWA JELA MIAKA 5….

Mahakama nchini Korea Kusini imemhukumu bilionea anayetarajiwa kurithi kampuni Samsung Lee Jae-yong kifungo cha miaka mitano jela kwa makosa ya utoaji rushwa.

Bw Lee alikuwa ameshtakiwa kuhusika katika rushwa katika kashfa ambayo pia ilichangia kuondolewa madarakani kwa rais wa zamani wa Korea Kusini.
Kesi hiyo ilikuwa imevutia sana umma huku hasira zikiendelea kupanda dhidi ya kampuni kubwa za kibiashara za Korea Kaskazini, maarufu kama chaebols.
Bw Lee, ambaye amekanusha mashtaka yote, alikuwa amekabiliwa na uwezekano wa kufungwa jela hadi miaka 12.
Bw Lee, ambaye pia hufahamika kama Jay Y Lee na amekuwa ndiye kiongozi wa kampuni hiyo kubwa zaidi ya kuunda simu duniani, amekuwa kizuizini tangu Februari akikabiliwa na tuhuma kadha za rushwa.
Miongoni mwa makosa aliyokabiliwa nayo ni utoaji rushwa, wizi wa mali ya umma na kuficha mali nje ya nchi.
Lee, 49, pia alituhumiwa kutoa mchango wa hisani wa won 41bn ($36m; £29m) kwa nyakfu za hisani zilizosimamiwa na rafiki wa karibu wa rais aliyeondolewa madarakani Park Geun-hye, ndipo apendelewe kisiasa.
Waendesha mashtaka wanasema mchango huo ulitolewa kwa mwandani mkuu wa Bi Park ili serikali iunge mkono mageuzi katika mfumo wa usimamizi wa kampuni ya Samsung ambao ungempatia Lee nguvu zaidi katika udhibiti wa kampuni ya Samsung Electronics.
Wakili wa Lee amesema tayari kwamba watakata rufaa uamuzi huo.

Uamuzi huo wa mahakama ni pigo kubwa kwa kampuni hiyo kubwa zaidi na inayofahamika zaidi ya Korea Kusini.

0 comments:

Post a Comment