Thursday 24 August 2017

RAIS AIDHINISHA HIFADHI KUBWA ITUMIWE KWA UCHIMBAJI MADINI…

Serikali ya Brazil imefutilia mbali hifadhi kubwa ya taifa katika eneo la Amazon ili kutoa fursa ya uchumbaji wa madini katika eneo hilo.

Hifadhi hiyo, yenye ukubwa wa kilomita 46,000 mraba (maili mraba 17,800) hupatikana katika majimbo ya kaskazini ya Amapa na Para na inaaminika kuwa na dhahabu pamoja na madini mengine.
Serikali imesema maeneo tisa ya uhifadhi na ardhi inayolindwa ya watu asilia, ambayo yanapatikana ndani ya hifadhi hiyo, yataendelea kulingwa kisheria.
Lakini wanaharakati wa hutetea uhifadhi wa utamaduni na mazingira wamelalamika kwamba maeneo hayo yataathirika pakubwa.
Kwa jumla, inakadiriwa kwamba 30% ya eneo lote la hifadhi hiyo litatumiwa kwa uchimbaji wa madini.
Agizo rasmi kutoka kwa Rais Michel Temer lilifutilia mbali hifadhi hiyo ambayo hufahamika kama Hifadhi ya Taifa ya Shaba Nyekundu na Washirika (Renca).
MaurĆ­cio Voivodic, mkuu wa shirika la uhifadhi wa wanyama la WWF nchini Brazil, alitahadharisha mwezi jana kwamba uchimbaji wa madini katika eneo hilo utasababisha "ongezeko kubwa la watu, ukataji mkubwa wa miti, kuharibiwa kwa chemchemi, kupotea kwa viumbe na miti pamoja na kuzuka kwa mizozo kuhusu ardhi".
Wizara ya madini na nishati nchini Brazil ilipendekeza kufutwa kwa hifadhi hiyo ili kuchochea maendeleo eneo hilo.
Kwa mujibu wa ripoti ya WWF, eneo kuu ambalo litatumiwa kwa uchimbaji wa madini ya shaba nyekundu na dhahabu litakuwa ndani ya eneo moja miongoni mwa maeneo yanayofaa kulindwa, ambalo huitwa Hifadhi ya Viumbe ya Maicuru.
Inasadikika kwamba kuna dhahabu pia katika msitu wa Para, ambao unapatikana ndani ya hifadhi hiyo.
WWF wanasema kuna uwezekano wa kuzuka kwa mizozo katika hifadhi mbili za watu asilia ambazo ni makao ya jamii ambazo zimekuwa zikiishi bila kuingiliwa na watu kutoka nje.

Ripoti ya WWF imesema 'mbio za kukimbilia dhahabu' eneo hilo zinaweza kuharibu utamaduni wa watu hao.

0 comments:

Post a Comment