Mahakama
ya Juu nchini Kenya imeukubalia muungano wa upinzani nchini humo National Super
Alliance (Nasa) kupekua sava zilizotumiwa na tume ya uchaguzi nchini humo
wakati wa uchaguzi uliofanyika tarehe 8 Agosti.
Mahakama hiyo imesema muungano
huo utaweza kusoma data kwenye sava hizo chini ya uangalizi kuhakikisha usalama
wa mitambo ya IEBC hauhujumiwi.
Mgombea wa Nasa Raila Odinga
amewasilisha kesi mahakamani kupinga ushindi wa Rais Uhuru Kenyatta wa chama
cha Jubilee.
Mawakili wa Bw Odinga
wameruhusiwa na mahakama kunakili data kutoka kwenye sava hizo kwa ajili ya
kufanya uchunguzi kuhusu uchaguzi huo.
Miongoni mwa mengine, upinzani utapata utambulisho wa
sava zilizotumiwa wakati wa uchaguzi, ukuta wa kinga uliotumiwa kulinda sava
hizo pamoja na mitambo ya dijitali ya uchaguzi wa Kenya (KIEMS) dhidi ya
wadukuzi na mfumo endeshi wa mitambo hiyo pamoja na nywila zilizotumiwa kuingia
katika mitambo hiyo.
Kadhalika, wataweza kupata
taarifa kuhusu yaliyojiri katika mitambo hiyo ya uchaguzi kuanzia Agosti tano
hadi leo.
Aidha, wataruhusiwa kusoma nakala
za Fomu 34A na 34B (fomu za matokeo katika vituo vya kupigia kura na ngazi ya
maeneo bunge) ambazo zilitumiwa kutangaza matokeo.
Taarifa kuhusu mchakato wa
upinzani kupekua sava na mitambo hiyo ya IEBC itawasilishwa kwa mahakama hiyo
kesho jioni.
Majaji saba wa mahakama hiyo ya
juu wameanza kusikiliza kesi hiyo iliyowasilishwa na Bw Odinga leo.
Kwa mujibu wa matokeo ya IEBC,
Rais Kenyatta alipata kura 8,203,290 huku naye Raila Odinga akipata kura
6,762,224.
0 comments:
Post a Comment