Jeshi la Polisi nchini Tanzania linaendelea na msako mkali kuwatafuta
watu waliompiga risasi na kumuua Mkurugenzi na Mwanzilishi-Mwenza wa Shirika
lisilo la kiserikali la PAMS Foundation, Wayne Lotter jijini Dar es Salaam
juzi.
Kwa mujibu
wa vyanzo vya habari nchini Tanzania Lotter ndiye aliyekuwa amewezesha
kukamatwa kwa mfanyabiashara, Yang Feng Glan maarufu kama ‘Malkia wa Meno ya
Tembo’ hivi karibuni baada ya mhalifu huyo kusakwa kwa muda mrefu katika
mataifa mbalimbali duniani kwa kuhusika na biashara ya meno ya tembo.
Kwa upande
wake Waziri wa Maliasili na Utalii Profesa Jumanne Maghembe ameeleza
kusikitishwa na tukio hilo la mauaji hayo ya mwanaharakati huyo.
Akitoa
taarifa kwa waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Kaimu Kamanda Kanda
Maalumu, Lucas Mkondya amesema tukio hilo lilitokea Agosti 16, saa tano maeneo
ya makutano ya barabara ya Haile Selassie na Kaole eneo la Masaki.
Taarifa
kutoka eneo la tukio zinasema Lotter (miaka 51), alipigwa risasi katika maeneo
hayo ya Masaki, wakati akitokea Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere
(JNIA) ambapo teksi aliyopanda ilisimamishwa na gari lingine kabla ya watu
wawili kuteremka na kumpiga risasi.
Lotter
alikuwa Mkurugenzi na Mwanzilishi-Mwenza wa PAMS Foundation, Shirika lisilo la
Kiserikali ambalo linajihusisha na masuala ya kupinga ujangili ambalo lilianza
shughuli zake Tanzania mwaka 2009.
Duru za
harakati za kulinda mazingira zimeeleza kuwa Lotter alikuwa amepanga kufanya
mikakati mbalimbali ya kukabiliana na ujangili wa tembo ikiwemo kuzindua vilabu
vya kupinga ujangili, kufunga vifaa vya GPS kwa tembo wote nchini, pia alikuwa
msaada kwa serikali kupitia miradi mbali mbali kama vile kufanikisha kumkamata
malkia wa ndovu aliyekuwa anatafutwa Dunia nzima ambaye alikamatwa nchini miezi
michache iliyopita.
Pia
alianzisha vikosi vya ulinzi (game rangers) ambao aliwalipa ili kusaidia ulinzi
wa tembo kwenye mbuga mbalimbali nchini. Alifadhili pia filamu ya The Ivory
Game iliyochezewa Tanzania na China, ambayo ilizinduliwa Hollywood, Marekani
ikionesha ujangili unavyofanyika na pia alisaidia magari ya doria kwa Jeshi la
Polisi na Wizara ya Maliasili na Utalii.
Polisi
imesema wauaji hao wanaodhaniwa kuwa ni majambazi mbali na kumuua mkuregenzi
huyo, walipora kompyuta mpakato tatu, simu moja aina ya Nokia na nyaraka
mbalimbali.
0 comments:
Post a Comment