Thursday 31 August 2017

CHUO CHATUMA DOLA MILIONI MOJA KWA MWANAFUNZI KIMAKOSA AFRIKA KUSINI….

Chuo Kikuu kimoja nchini Afrika Kusini kimesema kwamba kilituma kimakosa jumla ya randi milioni 14 ambazo ni sawa na dola milioni moja za Marekani katika akaunti ya benki ya mwanafunzi mmoja nchini humo.

Pesa hizo zilitoka kwenye mfuko wa shirika la kufadhili wanafunzi kimasomo nchini humo NSFAS.
Chuo Kikuu cha Walter Sisulu, kinasema kuwa pesa hizo ziliwekwa miezi mitano iliyopita, huku makosa hayo yakijulikana baada ya risiti ya akaunti ya mwanafunzi huyo kuonyesha kuwa na mamilioni ya pesa baada ya kuwekwa katika mtandao wa kijamii.
Chuo hicho kikuu sasa kinachunguza ni kwa nini mwanafunzi huyo hakupiga ripoti ya kuwepo kiasi kikubwa hivyo cha pesa kwenye akaunti yake.
Mwanafunzi huyo amekanusha madai hayo.
Ripoti ya shirika la habari la EWN inasema picha zimeonekana kwenye mitandao ya kijamii, zikionyesha mwanafunzi huyo wa kike huyo akijisifu na kujionyesha kwenye sherehe moja huku akijiburudisha na vitu vizuri vizuri, kama vile simu mpya ya rununu.
Inaaminika kwamba mwanafunzi huyo tayari ametumia randi 400,000.
Msemaji wa Chuo hicho Kikuu Yonela Tukwayo amesema kuwa, pesa hizo ziliwekwa kwenye akaunti hiyo kimakosa na kampuni ambayo inasimamia fedha za hazina ya kitaifa za msaada wa karo ya wanafunzi (NSFAS) ambayo inajulikana kama Intellicard na kwamba ni sharti mwanafunzi huyo arejeshe fedha hizo.


0 comments:

Post a Comment