Thursday 17 March 2016

HOSPITALI ZATUMIA MAJI YENYE VINYESI…

Utafiti uliofanywa umebaini kuwa asilimia 46.5 ya hospitali hapa nchini, zinatumia maji yenye vimelea vya kinyesi (Ecoli).

Kauli hiyo ilitolewa juzi jijini Dar es Salaam na mtafiti ambaye pia ni mtaalamu wa mazingira kutoka Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Robert Njee, katika mafunzo kwa waandishi wa habari kuhusu usafi wa mazingira na maji.
Amesema hayo yamebainika katika utafiti uliofanyika mwishoni mwa mwaka jana ukihusisha wilaya saba, huku Hospitali ya Wilaya ya Mbarali mkoni Mbeya inaongoza kwa kuwa na matumizi ya maji yenye vimelea vya kinyesi (Ecoli) kwa asilimia 57.9.
Njee amesema kuwa hospitali za wilaya za Temeke Dar es Salaam na Mufindi mkoani Iringa, zinashika nafasi ya pili katika matumizi ya maji yasiyo salama kwa asilimia 57.1 zikifuatiwa na Hospitali ya Mkoa wa Mbeya yenye asilimia 45.5.
Amezitaja hospitali nyingine kuwa ni Makete yenye asilimia 40.7, Njombe asilimia 38.1 pamoja na Iringa yenye asilimia 30.8.
Mtaalamu huyo wa mazingira aesema kuwa wilaya hizo saba zilifanyiwa utafiti, kwa lengo la kuunga mkono Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto ,katika kuboresha huduma za afya kupitia unawaji, utoaji wa huduma kwa mama na mtoto na kudhibiti utumiaji wa maji.

Njee amesema lengo jingine lilikuwa ni kuangalia na kutathimini utoaji wa huduma kwa jamii, kwa kuzingatia usafi wa mazingira pamoja na utakasaji mikono.

0 comments:

Post a Comment