Wednesday 6 April 2016

TOP 5 YA WEZI WAPUMBAVU DUNIANI…

Katika karibu kila jambo duniani, mwanadamu huhitajika kutumia akili ili kufanikiwa.

Bila shaka iwapo utatarajia uwazidi watu wengine hasa katika kuwapora au kuwaibia basi utahitajika kuwa na ujanja zaidi.
Lakini maeneo mbalimbali duniani kunao wahalifu ambao walionekana kupungukiwa ujanja.
Majuzi kwa mfano wanaume wawili kutoka Skegness Lincolnshire, walijipiga picha wakiimba pesa kutoka kwenye mitambo ya kucheza Kamari Bradford, Uingereza.
Hawakuenda mbali kwani walikamatwa muda mfupi baadaye Benjamin Robinson 30, alifungwa jela miezi 32 naye Daniel Hutchinson,akahukumiwa kifungo cha miezi sita jela ambacho kimeahirishwa.
Hao hawako peke yao hapa nimekuwekea listi ya wahalifu wengine waliojichongea:
1. Jambazi aliyejitapa Facebook
Andrew Hennells alikamatwa baada ya kuandika kwenye Facebook akijisifu kuhusu mpango wake wa kushambulia duka la jumla la Tesco eneo la King's Lynn Norfolk.
Aliweka kwenye Facebook picha yake ya kujipiga yaani ‘selfie’, picha ya kisu na kuandika: "Doing Tesco Over." (Nafanya Tesco Twende).
Alikamatwa na polisi dakika 15 baadaye akiwa na kisu chake na pesa £410 alizoiba.
Alifungwa jela miaka minne Aprili mwaka jana.
2. Mwizi aliyetekwa na usingizi
Wachumba katika eneo la Lancashire walirejea kutoka likizoni mwaka 2014 na kumpata mwizi amelala usingizi wa pono katika kitanda chao.
Martin Holtby and Pat Dyson walishangaa kumpata mwizi huyo Lukasz Chojnowski, alikuwa ameosha vyombo, akafua nguo zake za ndani na hata kununua mboga.
Wanasema nyumba yao haikuwa safi sana walipoondoka kwenda likizoni.
Walimpata Chojnowski aliyetoka Poland lakini akahamia Leeds, alikuwa amefanya usafi vilivyo.
Chojnowski 28 alikiri kosa la kuvunja nyumba na akatakiwa kukaa miaka miwili bila kutenda kosa na kulipa gharama ya £200.
3. Mwizi wa benki aliyeacha anwani yake

Mwizi wa benki aliyejaribu kujificha kwa kuvalia miwani ya giza n ahata kuvalia soksi juu ya viatu vyake, alisahau kwamba alikuwa ameacha anwani yake.
Dean Smith 27 alikuwa ameenda kwenye tawi la benki ya Barclays eneo la Treorchy, Wales kubadilisha anwani yake alipovutiwa na pesa zilizokuwa kwenye meza.
Alirejea baadaye akiwa amevalia miwani hiyo ya giza na soksi na kumtaka keshia ampe pesa hizo.
Keshia alikataa na akalazimika kutoroka mikono mitupu. Polisi walimpata kwa njia rahisi baada ya kufuatilia video ya kamera ya CCTV, wakamtambua na kisha kufahamu anwani yake.
Alikiri kwamba alikuwa “mjinga sana” na alifungwa miaka miwili unusu.
4. Mwizi aliyewatumia polisi picha nzuri
Mwanamume aliyekuwa akisakwa kwa makosa ya kuteketeza na kuharibu mali alituma picha ya selfie kwa maafisa wa polisi akisema picha iliyotumiwa na maafisa hao katika tangazo la kutafutwa kwake haikuwa ya kupendeza.
Donald "Chip" Pugh aliwatumia maafisa wa polisi picha aliyojipiga mwenyewe na kuandika ujumbe unaosema: "Hii hapa picha yangu nzuri, hiyo mliyotumia ni mbaya sana”.
Polise katika mji wa Lima jimbo la Ohio, walikuwa wamepakia picha kwenye ukurasa wao wa Facebook wakiomba msaada wa kumtafuta Bw Pugh.
Polisi walimjibu na kusema angefanya hisani zaidi kwa kujifikisha kwao,hata hivyo alikamatwa baadaye katika  jimbo la Florida.
5. Gaidi aliyejitokeza kudai zawadi
Maafisa nchini Afghanisan waliachwa vinywa wazi baada ya kamanda mmoja wa kundi la Taliban kujisalimisha na kisha kujaribu kudai zawadi ya $100 iliyokuwa imeahidiwa mtu ambaye angesaidia kukamatwa kwake.
Mohammad Ashan alituhumiwa kupanga mashambulio dhidi ya wanajeshi wa Marekani na Afghanistan mashariki mwa nchi hiyo.
Ripoti zinasema alifika katika kizuizi cha polisi mwaka 2012, akaelekeza mkono wake kwenye bango lenye picha yake na kisha akadai zawadi hiyo ya $100.

Maafisa wa usalama walishangaa sana na kushindwa kuelezea kitendo chake. Afisa mmoja wa Marekani anadaiwa kuambia wanahabari: “Kusema kweli, mwanamume huyu ni mpumbavu.”

0 comments:

Post a Comment