Serikali
ya Venezuela imeagiza wafanyakazi wake wawe wakifanya kazi siku mbili kwa
wiki,hii ni hatua ya muda iliyochukuliwa
kutokana na uhaba wa umeme.
Makamu wa Rais Aristobulo Isturiz ametangaza kwamba,
watumishi wa umma wanafaa kufika kazini Jumatatu na Jumanne pekee hadi mzozo wa
sasa wa nishati umalizike.
Venezuela imekabiliwa na ukame
mkubwa, ambao umepunguza maji kwenye bwawa lake kuu la kufulia umeme.
Lakini upinzani umeituhumu
serikali kwa kutodhibiti vyema mzozo wa sasa.
Agizo la kupunguzwa kwa siku za
kufanya kazi, lililotolewa kupitia runinga ya taifa na Bw Isturiz litaathiri
watu milioni mbili wanaofanya kazi serikali.
Rais Nicolas Maduro tayari amewaruhusu wafanyakazi 2.8
milioni wa serikali nchini humo, kutofanya kazi Ijumaa mwezi Aprili na Mei, ili
kupunguza matumizi ya umeme.
Amesema Venezuela imeathiriwa
sana na hali ya hewa ya El Nino, na kwamba hali ya kawaida itarejea baada ya
mvua kuanza kunyesha.
Serikali imekuwa ikichukua hatua
mbalimbali kupunguza matumizi ya umeme.
Mwezi Februari maduka yaliagizwa kupunguza muda ambao
yanafunguliwa kila siku, na pia kujaribu kujizalishia umeme.
0 comments:
Post a Comment