Friday 5 June 2015

Data za wafanyakazi milioni 4 zadukuliwa Marekani….!!!



Serikali ya Marekani imethibitisha habari ya kudukuliwa taarifa za karibu wafanyakazi milioni nne wa serikali ya nchi hiyo.
Shirika la habari la Ufaransa limeinukuu serikali ya Marekani ikisema kuwa,wadukizi katika mitandao ya Intaneti wamedukiza taarifa za karibu wafanyakazi milioni nne wa zamani na wa hivi sasa wa serikali ya nchi hiyo.

Kwa mujibu wa ripoti hiyo idara ya masuala ya wafanyakazi ya Marekani, mwezi Aprili mwaka huu iligundua kuwa, taarifa za wafanyakazi milioni nne wa serikali ya nchi hiyo zimedukuliwa.

Ripoti hiyo imeongeza kuwa, hadi sasa haijajulikana iwapo wafanyakazi wa ngazi za juu wa Marekani ni miongoni mwa watu waliodukuliwa taarifa zao au la.

Gazeti la Washington Post limewanukuu viongozi wa serikali ya Marekani wakidai kuwa, wadukizi kutoka China ndio waliofanya udukizi huo.

Hata hivyo ubalozi wa China mjini Washington umekanusha vikali madai hayo,na kusema kuwa kauli hizo za viongozi wa Marekani ni za kukurupuka.

Msemaji wa ubalozi huo Zhu Haiquan amesema kuwa, China inafanya juhudi kubwa za kupambana na udukizi mitandaoni, na kwamba si jambo jepesi kuweza kufuatilia na kugundua matukio kama hayo ambayo yanafanyika ndani ya mipaka ya nchi nyingi duniani.

0 comments:

Post a Comment