Monday 1 June 2015

Ujerumani ina idadi ndogo zaidi ya watoto duniani...!!



 
Idadi ya watoto wanaozaliwa nchini Ujerumani imepungua zaidi ya mataifa yote duniani.

Utafiti umeonesha kuwa idadi ya watoto wanaozaliwa nchini Ujerumani ndiyo ya chini zaidi duniani na sasa kunahofu kuwa kupungua kwa uzazi kutaathiri pakubwa uwezo wa vijana kuendeleza kasi ya ukuaji wa uchumi wa taifa hilo tajiri zaidi barani Ulaya.
Watafiti wanaonya kuwa endapo jitihada mahsusi hazitafanywa ilikuimarisha idadi ya watoto nchini humo basi uchumi wa taifa hilo utaathirika vibaya.
Kulingana na utafiti huo,watoto 8.2 pekee walizaliwa miongoni mwa watu wazima 1000.
Awali idadi ya chini zaidi ilikuwa ya Japan ambayo huandikisha idadi ya watoto 8.4 wanaozaliwa miongoni mwa watu wazima 1000.
Kampuni ya uhasibu ya Ujerumani BDO ikishirikiana na chuo cha utafiti wa kiuchumi cha Hamburg Institute of International Economics (HWWI) ndiyo iliyoendesha utafiti huo kwa lengo la kutathmini uwezo wa uchumi wa taifa hilo kujiendesha mbali na viwango vya uzazi vinavyoripotiwa nchini humo.
Barani Ulaya, Ureno na Italia ziliorodheshwa katika nafasi ya tatu na nne zikiwa na jumla ya watoto 9.0 na 9.3 mtawalia.
Ufaransa na Uingereza zinasajili watoto 12.7 wanaozaliwa miongoni mwa watu wazima 1000.
Niger iliyoko Afrika ndiyo inayoandikisha idadi kubwa zaidi ya watoto wanaozaliwa duniani.
Nchini humo watoto 50 huzaliwa miongoni mwa watu wazima 1000.
Kulingana na utafiti huo wa BDO iwapo hali itaruhusiwa kuendelea hivyo basi idadi ya watu wenye umri wa kati ya miaka 20 na 65 wenye uwezo wa kufanya kazi na uwezo wa kuendesha uchumi wa taifa hilo itapungua kwa asilimia 61% hadi 54% ifikapo mwaka wa 2030.
Aidha afisa wa BDO Arno Probst, aliwatahadharisha wajerumani kuwa kiwango cha malipo na mishahara ya wafanyikazi kitaongezeka maradufu kadri ya upungufu wa watu wenye uwezo wa kufanya kazi .
Probst alisema Ujerumani italazimika kuwaruhusu wahamiaji kuingia nchini humo na kufanya kazi ilikuepuka kuzorota kwa uchumi wake.

0 comments:

Post a Comment