Tuesday 16 June 2015

Unafahamu kwa nini kuna siku ya mtoto wa Africa…!!!



Tarehe 16 Juni ya kila mwaka Tanzania huungana na Nchi nyingine za Afrika kuadhimisha Siku ya Mtoto wa Afrika.

Mnamo mwaka 1990 uliokuwa Umoja wa Nchi Huru za Afrika (OAU),ulipitisha Azimio la kuwakumbuka watoto wa kitongoji cha Soweto kilichopo Afrika ya Kusini, waliouawa kinyama na iliyokuwa Serikali ya Makaburu ya nchi hiyo tarehe 16 Juni 1976.
Watoto hao walikuwa wakidai haki ya kutobaguliwa na haki nyingine za kibinadamu.
Hivyo OAU iliazimia kuwa tarehe 16 Juni ya kila mwaka iwe Siku ya Mtoto wa Afrika na nchi zote wanachama wa AU ziadhimishe siku hii.
Madhumuni mengine ni kusisitiza wajibu wa Serikali za Afrika kwa watoto, kuandaa na kutekeleza mipango ya wadau kuwaendeleza watoto,Kuinua kiwango cha uelewa na ufahamu wa jamii kuhusu matatizo yanayowakabili watoto wa Afrika na kuyatafutia ufumbuzi.

Tanzania kama mwanachama wa Umoja wa Afrika, imekuwa ikiadhimisha siku hii kwa miaka ishirini na tatu (23) tangu mwaka 1991, ikitumia siku hii kutafakari kwa kina matatizo yanayowakabili watoto na kutafuta namna ya kuyapatia ufumbuzi matatizo hayo.
Hapa Tanzania mwaka huu maadhimisho haya yanafanyika katika ngazi ya Mikoa,ili kuimarisha juhudi za wadau mbalimbali katika kulinda na kuendeleza haki na maslahi ya watoto nchini.

Kaulimbiu ya Maadhimisho ya Siku ya Mtoto wa Afrika mwaka 2105 ni “Tokomeza Mimba na Ndoa za Utoton, Kwa Pamoja Tunaweza

Kaulimbiu hii inalenga kukumbusha wazazi, walezi, serikali na jamii kwa ujumla kuhakikisha kuwa watoto hawaolewi katika umri mdogo kwa kuwa kufanya hivi kunawanyima haki yao ya msingi ya kuendelea na masomo na hatimaye kuishi maisha ya ufukara.

0 comments:

Post a Comment