Tuesday 14 February 2017

KWA UDANGANYIFU KWENYE MITIHANI..

Mahakama ya Juu nchini India imefuta leseni za madaktari 634 ambao wamejipata kwenye sakata ya wanafunzi kutumia udanganyifu kujiunga na vyuo vya mafunzo ya udaktari katika jimbo la Madhya Pradesh.

Mamia ya wanafunzi, imebainika, walitumia udanganyifu kujiunga na vyuo vya mafunzo ua udaktari kati ya 2008 na 2013.
Maelfu ya watu wamekamatwa kuhusiana na kashfa hiyo ambayo imepewa jina Vyapam
Vyapam ni ufupisho wa afisi ya serikali ambayo husimamia mitihani kabla ya watu kupewa kazi za serikali au kujiunga na vyuo majimbo nchini India.
Kwenye uamuzi wake, Mahakama ya Juu imesema waliofutiwa leseni walijihusisha katika "vitendo vya udanganyifu" na "ulaghai wa kiwango kikubwa".
Kashfa hiyo ilihusisha kuvujishwa kwa karatasi za mitihani, kudanganya kupitia karatasi za majibu ya mitihani na pia kukodishwa kwa wanafunzi werevu kufanyia mitihani watahiniwa wengine.
Kadhalika, nafasi za kuingia vyuoni viliuziwa watu walioweza kulipa pesa nyingi.
Waandishi wa habari wanasema nafasi moja chuoni iligharimu kati ya rupia 1 milioni ($15,764; £10,168) na rupia 7m.
Watu zaidi ya 2,000 wametuhumiwa kuhusika katika kashfa hiyo tangu 2012.

Watu 33, wengi wao wakiwa watuhumiwa katika kashfa hiyo, wamefariki katika hali ya kutatanisha katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita.

0 comments:

Post a Comment