Friday 3 February 2017

MBOWE NA NAIBU SPIKA DR TULIA NDANI YA BIFU JIPYA

Mvutano umeibuka bungeni kati ya Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani, Freeman Mbowe na Naibu Spika, Dk Tulia Ackson baada ya Mbunge huyo wa Hai kumwuliza Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa swali lililopingwa na Naibu Spika kwa maelezo kuwa ni la kisheria si la kisera.


Sakata hilo liliibuka asubuhi katika kipindi cha maswali kwa Waziri Mkuu, baada ya Mbowe kuhoji sababu za Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema kusota rumande kwa kukosa dhamana, Peter Lijualikali wa Kilombero anayetumikia kifungo cha miezi sita gerezani na wanachama wengine wa Chadema wanaokabiliwa na mashitaka mbalimbali.

Mbowe alimtaka kiongozi huyo wa shughuli za Serikali bungeni, aeleze kama ni sera ya Serikali kuua vyama vya upinzani, huku akisema Rais John Magufuli alipata kutamka kuwa atavimaliza vyama vya upinzani kabla ya mwaka 2020.

Kwa maswali hayo, Dk Tulia alimtaka Waziri Mkuu kujibu swali linalohusu sera na kuachana na yanayogusa masuala ya kisheria.

Jambo hilo liliwafanya wabunge wa Upinzani huku wakipiga meza kwa takribani dakika tano kupinga, wakimtaka Naibu Spika aache Waziri Mkuu ajibu swali hilo.

Katika swali lake la msingi, Mbowe alisema wakati jana ikiwa ni Siku ya Haki Duniani, imepita miezi mitatu tangu Lema aanze kusota rumande huku akinyimwa dhamana licha ya kuwa iko wazi.

Pia alisema Lijualikali anatumikia kifungo cha miezi sita jela kwa kosa la kisiasa sambamba na mwenyekiti wa chama hicho wa mkoa wa Lindi, Suleiman Mathew aliyefungwa miezi minane na madiwani zaidi ya sita na viongozi wengine 215 nao wakifungwa au kuendelea na mashitaka huku zikifanyika hila za kuidhoofisha CUF.

“Haya yanayoendelea katika Serikali ambayo ni kinyume na utamaduni na mazoea yetu kama Taifa, je ni utekelezaji wa sera ya kuua upinzani chini ya Rais Magufuli?” Alihoji Mbowe.

Kabla ya Waziri Mkuu kujibu swali hilo, Dk Tulia aliingilia kati na hali kuwa hivi:

Dk Tulia: Katika swali lako kuna masuala ya kisera na kisheria. Maswali yanayomhusu Lema na Lijualikali na madiwani sita ni ya kisheria, hayo kuhusu leo (jana) kuwa siku ya haki duniani, Waziri Mkuu anaweza kuyajibu.

Majaliwa: Nakanusha, Rais hajawahi kutangaza kuvifuta vyama vya upinzani, nchi inaongozwa kwa sheria, kanuni na taratibu na kuna Bunge, Serikali na Mahakama.Hakuna mhimili unaoingilia mhimili mwingine. Jambo lililopo mahakamani halizungumzwi kokote, siwezi kuzungumzia hilo.

Mbowe: Kwa kuwa Rais anaonekana kuvunja Katiba ikiwa ni pamoja na kupiga marufuku mikutano ya vyama vya siasa, je tukileta ushahidi kuwa Rais amekusudia kuumaliza upinzani kabla ya 2020, Waziri Mkuu utakuwa tayari kuwajibika kwa kujiuzulu?

Dk Tulia: Mbowe swali lako la maelezo ya jumla, yako sawasawa ila la kumtaka Waziri Mkuu kuwajibika si la kisera, kuwajibika si sera uliza swali la kisera.

Mbowe: Labda swali langu nilielekeze kwa Naibu Spika (Dk Tulia). Swali langu lilikuwa la mwendelezo ambalo hutokana na majibu ya msingi yaliyotokea. Kama kulikuwa na msingi wa kisera kwenye swali la msingi, swali la mwendelezo linakwenda kutokana na majibu yaliyotolewa. Waziri Mkuu aseme tu kama yupo tayari kujiuzulu tukileta ushahidi.


Katika maelezo yake, Dk Tulia alitaka Mbowe ajikite katika swali la kisera jambo ambalo Mwenyekiti huyo wa Chadema alipinga na kusisitiza kuwa huenda mambo yanayofanyiwa wapinzani, wabunge, mawaziri Serikali inayafurahia.

0 comments:

Post a Comment