Wednesday 1 February 2017

SERIKALI: UZALISHAJI WA CHAKULA UTAFIKIA TANI MILIONI 3

Serikali imefanya tathmini ya awali ya uzalishaji wa mazao ya chakula nchini na kubaini kuwa uzalishaji wa chakula nchini utakuwa na ziada ya tani 3,013,515.

Hayo yamesemwa Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, Dk Charles Tizeba amesema tathmini iliyofanywa, imebaini kwamba jumla ya tani 35,491 za chakula zinahitajika katika kukabiliana na hali ya upungufu wa chakula na lishe kati ya Februari na Aprili mwaka huu kwaajili ya watu 1,186,028 walioainishwa kuwa na upungufu katika halmashauri 55.
 Tizeba amesema kuwa ziada hiyo imebainika baada ya Bunge la 10 kutoa kauli ya kufanya tathmini ya upatikanaji na mahitaji ya chakula ambapo tathmini ya awali ya uzalishaji chakula kwa mwaka 2015/16 na upatikanaji wa chakula mwaka 2016/17, ilikamilika.
Aidha amesema kuwa tathmini hiyo imeonyesha kuwa kitaifa, uzalishaji wa chakula utafikia tani 16,172,841 za chakula na mahitaji ya chakula kwa mwaka huu ni tani 13,159,326 na hivyo kuwa na chakula cha ziada cha tani 3,013,515 yaani tani 1,101,341 ni mazao ya nafaka na tani 1,912, 174 ni za mazao yasiyo ya nafaka.

Hata hivyo amengeza kuwa tathmini hiyo ilishirikisha Shirika la Kilimo na Chakula Duniani (FAO) na Mpango wa Chakula Duniani (WFP) na wataalamu kutoka Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine (SUA) na Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) pamoja na Wizara ya Afya kupitia Taasisi ya Chakula na Lishe (TFNC).

0 comments:

Post a Comment